Burma: Kifungo cha Aung San Suu Kyi gerezani chapunguzwa hadi miaka miwili
Hukumu ya jela ya Aung San Suu Kyi, mwanasiasa wa zamani wa demokrasia nchini Burma aliyetunukiwa Tuzo ya Nobel mwaka 1991, kiongozi wa zamani wa nchi hii aliyepinduliwa Februari mwaka jana, imepunguzwa kutoka miaka minne hadi miwili, kiongozi wa utawala wa kijeshi ametangaza Jumatatu, baada ya tangazo la hukumu dhidi yake lililozua hisia mbalimbali nchini humo na nchi kadhaa duniani.
Imechapishwa:
Rais wa zamani Win Myint, ambaye alihukumiwa kifungo sawa na Aung San Suu Kyi , pia amejikuta kifungo chake kikipunguzwa hadi miaka miwili.
Win Myint na Aung San Suu Kyi walishtakiwa kwa kuchochea fujo za umma na kukiuka sheria za afya zinazohusiana na Covid-19. Mahakama ya Burma iliwahukumu, Jumatatu hii, Desemba 6, kifungo cha miaka minne jela kabla ya hukumu hizi kupunguzwa hadi miaka miwili na utawala aw kijeshi.
Kiongozi huyo wa zamani wa serikali mwenye umri wa miaka 76 bado anakabiliwa na mashtaka mengine.
Hukumu za awali zilizua wasiwasi mkubwa katika jumuiya ya kimataifa. Kamati inayotoa Tuzo ya Amani ya Nobel ilisema "ilikuwa na wasiwasi" kuhusu kiongozi huyo wa zamani wa Burma baada ya kuhukumiwa na utawala wa kijeshi.
Wasiwasi kwa mustakabali wa demokrasia nchini Burma
Katika taarifa iliyotumwa kwa shirika la habari la AFP, rais wa kamati ya Norway Berit Reiss-Andersen kwa ameeleza kwamba alikuwa na wasiwasi kuhusu "kufungwa huku kunamaanisha nini kwa mustakabali wa demokrasia nchini Burma", "wasiwasi juu ya uzito ambao kifungo cha muda mrefu kinaweza kumuathiri Aung San Suu Kyi kibinafsi ”.
"Kesi dhidi ya Aung San Suu Kyi inaonekana si ya kuaminika sana" na "ni sehemu ya ukandamizaji wa upinzani nchini Burma", anamshutumu rais wa kamati. Norway, kupitia sauti ya Waziri wake wa Mambo ya Nje, pia "imeshutumu vikali" kifungo chake cha jela na kutaka aachiliwe mara moja.
Washington yashutumu mahakama kuingiliwa kisiasa
Marekani pia imesema siku ya Jumatatu kwamba hukumu "isiyo ya haki" dhidi ya kiongozi wa zamani wa Burma Aung San Suu Kyi ilikuwa "unyanyasaji wa demokrasia na haki nchini Burma".
"Tunaitaka serikali kumwachilia Aung San Suu Kyi na wale wote waliozuiliwa kinyume na sheria, wakiwemo maafisa wengine waliochaguliwa kidemokrasia," Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken amesema katika taarifa yake.
"Kendele kudharau utawala wa sheria na matumizi makubwa ya unyanyasaji dhidi ya raia wa Burma kunasisitiza haja ya haraka ya kurejesha njia ya Burma kuelekea demokrasia", ameongeza Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani.
Aung San Suu Kyi ambae yuko chini ya kifungo cha nyumbani tangu mapinduzi
Huku akihukumiwa tangu Juni, Aung San Suu Kyi anashtakiwa kwa makosa mengi: uchochezi, rushwa, udanganyifu katika uchaguzi. Ana hatari ya kumaliza siku zake kizuizini.
Mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel ya 1991 amekuwa chini ya kifungo cha nyumbani tangu mapinduzi ya Februari 1, ambayo yalihitimisha ghafla mabadiliko ya kidemokrasia yaliyokuwa yakiendelea nchini Burma tangu mwaka 2010.
"Aung San Suu Kyi amejitolea maisha yake kupigania uhuru na demokrasia nchini Burma na ameshikilia jukumu hili gumu kwa zaidi ya miaka 30," kamati ya Nobel imesema.