Mazungumzo kati ya Korea Kaskazini na Korea Kusini yanaendelea
Wajumbe wa Korea Kaskazini na Kusini wameanza mazungumzo kuhusu namna wanamichezo wa Korea Kaskazini watakavyoshiriki katika michezo ya Olimpiki ya msimu wa baridi mwezi ujao.
Imechapishwa:
Mataifa hayo mawili wiki iliyopita, yalikubaliana kutuma wachezaji wa Korea Kaskazini watakaoshiriki katika michezo hiyo, hatua ambayo itasaidia kuimarisha uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.
Korea Kusini imekuwa ikitaka mazungumzo zaidi ikiwemo masuala ya usalama, lakini Korea Kaskazini imetaka mazungumzo hayo kuzingatia ushiriki wa wachezaji wake kuhusu michezo ya Olimpiki.
Mkutano huo unatarajiwa kufanyika katika eneo la Panmunjom, katika mpaka wa nchi hizo mbili, eneo ambalo linaelezwa la kihistoria kati ya nchi hizo mbili.
Mazungumzo ya mwisho kati ya nchi hizi mbili, yalifanyika mwaka 2015. Haijafahamika ni nani watakaohudhuria mazungumzo haya mapya.
Hatua hii, imeonekana kutuliza uhasama kati ya nchi hizi mbili, kutokana na mradi wa Korea Kaskazini kuzalisha silaha za nyuklia.
Korea Kaskazini imekuwa ikitishia kuishambulia Marekani na washirika wake kama Korea Kusini.
Rais wa Marekani Donald Trump amepongeza hatua hiyo ya kuwepo kwa mazungumzo hayo.