Shinikizo laongezeka kwa Myanmar kuhusu mgogoro wa jamii ya Rohingya
Mamia ya watu wa jamii ya Rohingya nchini Mynmar wakiwemo watoto na wanawake wanakosa mahitaji muhimu kama chakula na makaazi baada ya kukimbilia katika nchi jirani ya Bangladesh.
Imechapishwa:
Wanawake na watoto wameonekana wakinyeshewa mvua wakiwa katika mpaka wa Bangaldesha huku wakioneakania wakipata chakula na nguo kutoka kwa wasamaria wema.
Mashirika ya kutoa msaada yanasema kuwa watoto wawili wamepoteza maisha baada ya watu kukanyagana wakati wakipokea msaada wa chakula mwishoni mwa wiki iliyopita.
Watu 412,000 wa jamii ya Rohingya wanaolengwa na maafisa wa usalama katika nchi yao wamekimbia makwao na wanakabiliwa na mazingira magumu.
Suala la jamii ya Rohingya wanaoendelea kulengwa na kukimbilia nchi jirani linatarajiwa kupewa nafasi kubwa katika mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa huku ikitarajiwa kuwa mwafaka.
Mashirika ya kutetea haki za binadamu yanataka, jeshi la Mynmar kuwekewa vikwazo kwa kuwalenga waislamu ambao ni wachache nchini humo.
Kiongozi wa kiraia Aung San Suu Kyi ambaye hajakwenda jijini New York kuhudhuria mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, anatarajiwa kulihutibia taifa hapo kesho Jumanne kuhusu kinachotokea.