Korea Kaskazini yasema itaendelea na majaribio ya silaha zake wakati wowote
Korea Kaskazini imetangaza kuwa itaendelea na majaribio ya silaha zake za nyuklia wakati wowote, na katika eneo lolote.
Imechapishwa:
Tangazo hili limetolewa siku ya Jumatatu na serikali ya Pyongyang na kuzua hali ya wasiwasi katika eneo la Korea.
Wizara ya Mambo ya nje imesema jaribio hilo litafanyika wakati wowote lakini pia ikaongeza kuwa jeshi lake liko tayari kukabiliana na Marekani.
Korea Kaskazini imeendelea kutekeleza majaribio ya mashambulizi ya silaha zake mengine yakifanikiwa huku mengine yakishindwa.
Jeshi nchini humo kwa kipindi cha miaka 11 imefanya majaribio makubwa matano hatua ambayo imeikera serikali ya Marekani na Umoja wa Mataifa.
Rais Donald Trump ameonya kuwa ataishambulia Korea Kaskazini ikiwa itaendelea na majaribio haya hata bila ya msaada wa serikali ya China ambayo ni mshirika wa Pyongyang.
Beijing imekuwa ikisema kuwa ikiwa Marekani na Korea Kaskazini, zitashambuliana, hakuna atakayeibuka mshindi na hivyo imeendelea kutoa wito kwa mataifa hayo mawili kumaliza tofauti zao kwa njia ya mazungumzo.