Marekani kutoa msaada kwa Kenya katika mpango wake wa kurejesha utulivu Haiti
Utawala wa rais Joe Biden ameahidi msaada wa Dola milioni mia moja kupiga jeki juhudi ya Kenya kuongoza kikosi cha kimataifa kurejesha hali ya usalama nchini Haiti.
Imechapishwa:
Washington imetoa wito kwa kwa mataifa mengine kuunga mkono Kenya katika juhudi zake za kukabiliana na makundi ya magenge yanayoendelea kutatiza usalama wa raia katika taifa hilo la Haiti.
Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Antony Blinken amethibitisha kuwa Washington itatoa msaada wa usafiri, intelenjsia, matibabu na mawasiliano kwa ujumbe huo wa walinda amani. Mpango unafaa kuidhinishwa na baraza la usalama katika umoja wa mataifa.
Kando na Kenya ambayo itaoongoza ujumbe huo, Jamaica, Bahamas, Antigua na Barbuda zimeahidi kuwatuma wanajeshi wake.
Rais wa Kenya William Ruto amesema nchi yake imejitolea kuongoza kikosi cha kimataifa cha walinda amani nchini Haiti kama njia moja ya kurejesha hali ya utulivu na mpangilio kwenye taifa hilo.
Zaidi ya watu elfu ishirini, raia wa Haiti, wanaishi katika makaazi duni ya muda baada ya kutoroka makaazi yao kutokana na mashambulio ya magenge yenye silaha.
Magenge hayo pia yameripotiwa kutekea barabara muhimu kaskazini na kusini mwa Haiti, hali ambayo imetatiza usambazaji wa chakula.
Zaidi ya watu milioni nne nchini Haiti wanakabiliwa na tatizo la baa la njaa, watu milioni 1.4 wakiwa katika hatari kubwa.