Kesi ya mashtaka: Mawakili wa Trump walaani mchakato 'unaoongozwa na chuki'
Maseneta Nchini Marekani wanatarajia kukutana leo Jumamosi asubuhi kwa kuendelea na kesi inayomkabili aliyekuwa rais wa nchi hiyo Donald Trump. Kura juu ya kumtia hatia rais huyo wa zamani inaweza kufanyika wakati wa mchana.
Imechapishwa:
Donald Trump anatuhumiwa kuchochea vurugu. Wakati huo huo mawakili wake walijaribu kumtetea mteja wao jana Ijumaa. Walishutumu utaratibu unaokiuka katiba na walikanusha kuhusika kwa Donald Trump katika machafuko yaliyotokea katika makao makuu ya Bunge mnamo Januari 6.
"Mashitaka haya ambayo yako mbele ya Bunge la Seneti ni wazi kuwa ni kitendo cha ulipizaji kisasi kinachokiuka katiba" alisema Michael Van der Veen, mmoja wa mawakili wa Trump, huku akiitaja kesi hiyo kuwa inaongozwa na chuki dhidi ya mteja wake.
“Kwa bahati mbaya, kesi hii inahusiana na chuki za kisiasa.Ni wazi kabisa kwamba wabunge kutoka chama cha Democratic wanamchukia Donald Trump. Aina hii ya chuki ya kisiasa haina nafasi katika taasisi zetu za kisiasa na hakika haina nafasi katika sheria. Chuki ni kiini cha jaribio lisilokuwa na msingi la waendesha mashtaka kutoka chama cha Democratic kumfanya Donald Trump ahusishwe kwa vitendo vya uhalifu vya wafanya ghasia, kwa madai yasiyo kuwa ya kweli kutoka kwa makundi ya mrengo wa kulia, bila kuwa na ushahidi wowote wa kweli isipokuwa dhana mbaya tu. Chuki ni jambo la hatari. Chuki haipaswi kuwa na nafasi kwenye nafasi hii, katika utaratibu huu, " ameongeza
Waendesha mashtaka wa chama cha Democratic walikamilisha ushahidi wao dhidi ya Trump siku ya Alhamisi. Walihoji kuwa rais huyo wa zamani anawajibika moja kwa moja kwa uvamizi wa makao ya bunge, maarufu kama Capitol, na kulisihi baraza la seneti kumtia hatiani kwa kuchochea machafuko.