Trump awahimiza raia wake kuvaa barakoa katika maeneo ya umma
Rais wa Marekani Donald Trump sasa anasema janga la virusi vya Corona huenda likawa baya zaidi katika taifa hilo ambalo lina maambukizi karibu Milioni nne.
Imechapishwa:
Trump ambaye ameonekana kubadilisha mtazamo wake kuhusu janga hili, katika wito ambao pia haukutegemewa, amewataka Wamarekani kuvalia barakoa muda wote wanapokuwa katika maeneo ya umma, akisema kuwa ni ishara ya "uzalendo", jambo ambalo amesema yeye pia ameanza kufanya.
"Nitaivaa nikiwa kwenye kundi la watu, nikiwa na walinzi wangu nataka kuwalinda pia kwa hiyo nitavaa barakoa, sina tatizo na barakoa. Mtazamo wangu ni huu, kitu chochote kinachoweza kusaidia na bila shaka barakoa inaweza kusaidia, ni kitu kizuri. Sina shida, ninaibeba, ninaivaa, mumeniona nikiivaa mara kadhaa na nitaendelea," Rais Donald Trump amesema.
Donald Trump ameaonya kwamba “kwa bahati mbaya hali huenda ikawa mbaya zaidi kabla ya kuanza kubadilika.
Rais Donald Trump amekiri kuwepo na hatari ya janga la Covid-19 nchini Marekani.
"Kwa bahati mbaya, janga hili litazidi kuwa baya kabla ya hali kurejea kuwa shwari. Sijapenda kuzungumza hivyo lakini huo ndio ukweli, " amesema rais Donald Trump, kabla ya kutoa wito kwa kila mmoja 'kuvaa barakoa katika maeneo ya umaa'.
Kuikia sasa idadi ya maambukizi ya virusi vya Corona imepindukia milioni 14.9 na vifo vilivyotokana na virusi hivyo ni zaidi ya laki sita kote duniani wakati ambapo wanasayansi wako mbioni kutafuta chanjo.