Trump ajizuia kuzungumzia iwapo atakubali matokeo ya uchaguzi ujao wa urais
Rais wa Marekani Donald Trump amekataa kusema hadharani iwapo atakubali matokeo ya Uchaguzi wa urais utakaofanyika mwezi Novemba mwaka huu.
Imechapishwa:
Umaarufu wa Trump atakayepambana na Joe Biden wa chama cha Democratic, umepungua kutokana na namna serikali yake inavyopambana na maambukizi ya virusi vya Corona.
Katika mahoajiano na kituo cha Fox News, Trump amesema hawezi kusema iwapo atakubali matokeo hayo.
Hivi karibuni mshauri wa zamani wa usalama wa taifa wa Marekani alisema, ni jambo lililo mbali kwa Donald Trump kushinda tena katika uchaguzi wa rais wa nchi hiyo utakaofanyika mwezi Novemba mwaka huu.
John Bolton, ambaye katika wiki za karibuni amefichua mambo kadha yaliyoharibu na kuichafua shakhsia ya Donald Trump, amekosoa mtazamo na muelekeo wa rais huyo wa Marekani na kueleza kwamba, uwezekano wa yeye Trump kuendelea kusalia katika Ikulu ya White House unazidi kupungua.
Ikiwa imesalia miezi minne tu kabla ya kufanyika uchaguzi wa urais wa Marekani, hivi sasa Trump ametingwa na matatizo chungu nzima ya kiuongozi. Kutoridhishwa Wamarekani na jinsi Trump anavyoiongoza nchi kunashuhudiwa pia hata miongoni mwa waungaji mkono wake wa zamani ndani ya chama chake cha Republican.
Wakati huohuo chunguzi mbali mbali za maoni zinazoendelea kufanywa nchini Marekani zinaonyesha kuwa, kukubalika kwa Trump mbele ya wananchi kunazidi kupungua na endapo uchaguzi wa rais wa nchi hiyo utafanyika hivi sasa, mgombea urais kwa tiketi ya chama cha Democrat Joe Biden atamshinda vibaya Trump katika kinyang'anyiro hicho.