Mkataba wa Nyuklia wa Iran mashakani baada ya Tillerson kufutwa kazi
Hatua ya rais wa Marekani Donald Trump kumfuta kazi aliyekuwa Waziri wake wa Mambo ya kigeni Rex Tillerson tayari imeibua hofu kuhusu mustakabali wa mkataba wa nyuklia wa Iran uliotiwa saini na nchi za Magharibi ikiwemo Marekani.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Katika maelezo yake rais Trump amesema licha ya kuwa anampenda Tillerson, wamekuwa wakitofautiana katika masuala mtambuka ikiwemo mkataba wa nyuklia wa Iran na mazungumzo na Korea Kaskazini.
Akizungumza tangu kufutwa kwake kazi, Tillerson amewashukuru wafanyakazi wa wizara yake huku akijiepusha kumtaja rais Trump karibu katika sehemu yote ya hotuba yake ambapo ameongeza kuwa sasa anarudi kwenye maisha ya kiraia.
Aidha, ameishtumu Urusi kama nchi sumbufu ukiwa ni ujumbe wake wa mwisho baada ya kufutwa kazi.
Tayari rais Trump amemteua aliyekuwa mkurugenzi wa idara ya ujasusi ya Marekani CIA, Mike Pompeo kuwa waziri mpya wa Mambo ya kigeni na sasa anasuburi kuhojiwa na bunge kabla ya kuanza kwake kazi hiyo.
Kabla ya kufutwa kwake kazi, rais Trump alikuwa amemtuma Tillerson katika ziara ya kikazi barani Afrika nchini Kenya, Djibouti, Ethiopia, Chad na Nigeria.
Ripoti zinasema kuwa, hadi kufutwa kwake, Waziri huyo wa zamani ambaye zamani alikuwa Mfanyibiashara katika kampuni ya mafuta na gesi ExxonMobil.