Serikali nchini Mexico yawafukuza kazi maofisa 800 wa jeshi la polisi kwenye mji wa Veracruz
Serikali nchini Mexico imetangaza kuwafukuza kazi zaidi ya maofisa mia nane wa Polisi katika mji wa Veracruz ikiwa ni hatua za awali za kutaka kusafisha jeshi la nchi hiyo katika harakati za kupambana na makundi ya uuzaji wa dawa za kulevya.
Imechapishwa:
Msemaji wa Serikali ya Mexico, Gina Dominguez amesema kuwa mbali na kuwaachisha kazi maofisa hao wa polisi, ameongeza kuwa pia imewafukuza kazi viongozi wengine katika jeshi hilo zaidi ya mia tatu kutokana na tuhuma za kujihusisha na makundi ya dawa za kulevya.
Akiongea katika mkutano wake na waandishi msemaji huyo amesema kuwa polisi ambao wameachishwa kazi wanaweza kuomba tena nafasi hizo na wataajiriwa endapo wakifikisha vigezo vipya vya kujiunga na jeshi hilo vilivyotangazwa.
Hatua ya kuwafukuza kazi maofia hao zaidi ya mia nane ni ya kwanza kuwahi kuchukuliwa na Serikali ya nchi hiyo chini ya Utawala wa rais Felipe Caldrone ambaye ameahidi kupambana na makundi ya wauzaji wa dawa za kulevya nchini humo.
Tayari kikosi cha jeshi kimechukua madaraka ya kuongoza mji huo kwa muda ikiwa ni zoezi ambalo limezoeleka kwa vikosi vya jeshi la nchi kushika doria kwenye maeneo ambayo kuna wauzaji wengi wa dawa za kulevya.