Benin kuwatuma polisi 2,000 nchini Haiti chini ya kikosi cha kimataifa cha UN
Nairobi – Nchi ya Benin imesema itachangia maofisa wake wa usalama 2,000 katika kikosi cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa chini ya uongozi wa Kenya wanaotarajiwa kutumwa nchini Haiti kupambana na magenge yenye silaha.
Imechapishwa:
Hatua hiyo imethibitishwa hapo jana wakati wa taarifa kwa vyombo vya habari huko Georgetown, Guyana na balozi wa balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Linda Thomas-Greenfield.
Kwa mujibu wa Thomas-Greenfield, walifanya mazungumzo na waziri mkuu wa Haiti Ariel Henry na washirika wenginge kuhusu upelekaji wa vikosi hivyo nchini Haiti.
Aidha Thomas-Greenfield ameeleza kuwa ujumbe huo ni muhimu kwa ajili ya kuwasaidia polisi nchini Haiti kurejesha hali ya amani na usalama, kuchangia kufanyika kwa uchaguzi huru na haki pamoja na kuzuia kutokea kwa mzozo wa kibinadamu.
Polisi wa kimataifa wa kulinda amani walitakiwa kutumwa nchini Haiti mwezi huu lakini mchakato huo ulicheleweshwa kutokana na hatua ya mahakama nchini Kenya kuzuia mpango huo mwezi Januari.
Kwa mujibu wa uamuzi wa mahakama, serikali ya Kenya haikuwa na mamlaka ya kuwatuma maofisa wa polisi nje ya mipaka ya Kenya.
Mchafuko ya magenge ya watu wenye silaha yameongezeka zaidi nchini Haiti, visa vya utekaji nyara pia vikiripotiwa.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa ya mwezi uliopita ilieleza kuwa watu wenye silaha waliwaua raia 8,400 mwaka uliopita, ikiwa ni ongezeko la asilimia 122 kutoka mwaka wa 2022.