Comoros: Ushindi wa rais Azali Assoumani kupingwa mahakamani
Nairobi – Mwanasiasa wa upinzani katika visiwa vya Comoro na ambaye alikuwa miongoni mwa waliogombea katika uchaguzi mkuu wa urais, amewasilisha kesi mahakamani akitaka kubatilishwa kwa matokeo yaliompa ushindi rais wa sasa Azali Assoumani.
Imechapishwa:
Upinzani kwenye visiwa hivyo umepinga matokeo hayo ukisema kuwa uchaguzi huo haukufanyika kwa njia ya wazi hatua ambayo hata hivyo imesababisha maandamano makubwa kwenye kisiwa hicho.
Ushindi wa Assoumani unatarajiwa kuthibitishwa na mahakama ya juu wikendi hii baada ya tume ya uchaguzi kutangaza kuwa alipata zaidi ya asilimia 60 ya kura katika duru ya kwanza ya uchaguzi uliofanyika siku ya Jumapili.
Akizungumza nje ya mahakama ya juu zaidi kwenye kisiwa hicho, Daoudou Abdallah Mohamed, waziri wa zamani wa mambo ya ndani na ambaye aligombea kwa tiketi ya chama cha upinzani cha Orange, amesema tume ya uchaguzi ilichapisha matokeo bandia.
Mji mkuu wa Moroni umekabiliwa na makabiliano ya siku mbili kati ya maofisa wa polisi na waandamanaji waliokuwa wanapinga matokeo hayo ya urais.
Kwa mujibu wa takwimu rasimi, raia 189,497 wa Comoro walipiga kura kuwachagua magavana katika kila moja ya visiwa vitatu kwenye nchi hiyo, lakini ni 55,258 pekee walipiga kura kumchagua rais.
Assoumani mwenye umri wa miaka 65, afisa wa zamani wa jeshi anatuhumiwa kwa kuwafunga jela wapinzani wake ili kuendeleza ubabe wake madarakani.
Karibia asilimia 45 ya wakazi wa Comoro 870,000 wanadaiwa kuishi katika hali ya umaskini.