Tanzania: Rais Samia asitisha ziara yake Dubai baada ya mafuriko nchini mwake
Raia nchini Tanzania, wanaendelea kuomboleza kufuatia vifo vya watu zaidi ya 60 vilivyotokana na mafuriko na maporomoko ya udongo kwenye wilaya ya Hanang mkoani Manyara.
Imechapishwa:
Hili linafanyika wakati huu rais Samia Suluhu Hassan, akiwa amekatisha ziara yake mjini Dubai, alikokuwa akihudhuria mkutano wa kimataifa wa hali ya hewa COP28.
Rais Samia, ambaye alikuwa Dubai kuhudhuria mkutano wa COP28, atakuwa akielekea mji wa Katesh, kutathmini athari za baada ya mafuriko na maporomoko ya udongo.
Awali akizungumzia mkasa huo, rais Samia aliagiza taasisi za Serikali kuelekeza nguvu za uokoaji na utafutaji kwenye Wilaya ya Hanang, mkoani Manyara, ikiwemo kuzuia madhara zaidi.
Viongozi kadhaa wa Serikali walisafiri siku ya Jumapili kuelekea huko, ambapo pia tangu jana Jumatatu, waziri mkuu Kassim Majaliwa, alikita kambi huko kujionea zoezi la uokoaji na kuratibu shughuli nyingine ikiwemo zile za mazishi.
Kilichotokea nchini Tanzania, ni kile ambacho wanasayansi wanaoshiriki mkutano wa COP28 wanasema ni kutokana na athari za mabadiliko ya tabia nchi, wakitaka viongozi kuwajibika katika kuchukua hatua za kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.