Upigaji kura unaendelea nchini Zimbabwe kwa siku ya pili
Shughuli ya upigaji kura inaendelea katika baadhi ya sehemu nchini Zimbabwe baada ya tume ya Uchaguzi nchini humo kuongeza muda wa kupiga kura kumchagua rais na wabunge kuendelea leo, baada ya vituo vingi vya kupigia kura kutofunguliwa kwa wakati hapo jana hasa katika ngome za upinzani.
Imechapishwa:
Rais Emmerson Mnangagwa alitoa notisi kuwa upigaji kura utapanuliwa katika wadi 40, katika majimbo matatu kati ya 10. Inajumuisha sehemu za mji mkuu, Harare - ambao unachukuliwa kuwa ngome ya upinzani.
Ni robo tu ya vituo vya kupigia kura vilivyofunguliwa kwa wakati kutokana na matatizo ya karatasi za kupigia kura.
Katika baadhi ya maeneo, karatasi za kupigia kura ziliisha, na kuwalazimu wapiga kura kusubiri hadi usiku. Rais Emmerson Mnangagwa anatafuta muhula wa pili katika uchaguzi huu.
Mpinzani wake mkuu Nelson Chamisa kutoka chama kikuu cha upinzani cha CCC, anasema kuna njama za kuiba kura.
“Hatujafuraishwa na wanachofanya vijijini, ambako wanadhulumu watu na kusababisha vurugu na wanaweka kile kinachoitwa madawati ya uchunguzi wa kura, kwa kweli wanauliza watu ni wapi wamepiga kura na kuwaagiza wapiga kura kuhusu ni nani wanayefaa kumpigia kura.” alieleza Nelson Chamisa.
Nelson Chamisa, Kiongozi wa upinzani nchini Zimbabwe
Kiongozi huyo aidha alishutumu chama tawala cha Zanu-PF kwa kukandamiza zoezi la upigaji kura.
Wakati huo huo polisi wanaripotiwa kuvamia ofisi za waangalizi wawili huru wa ndani wa uchaguzi siku moja baada ya kupiga kura.
Kundi la kutetea haki za binadamu la Zimbabwe Lawyers for Human Rights, liliripoti kwamba idadi kubwa ya watu walizuiliwa na vifa vyao kuchukuliwa na maofisa wa polisi japokuwa hakuna uthibitisho kutoka kwa polisi.
Baraza la uchaguzi lina siku tano ya kutangaza matokeo ya uchaguzi wa urais.