Kenya: Uchunguzi wa miili ya Shakahola waondoa hofu ya uwepo wa biashara ya viungo vya binaadamu
Nairobi – Nchini kenya, uchunguzi uliofanywa kwa miili 112 ya watu waliofariki kutokana na kile kinachodaiwa kuwa maagizo ya mhubiri wao kufunga hadi kufa katika kaunti ya Kilifi Pwani ya Kenya, umefutilia mbali hofu iliyekuwepo kwamba huenda kulikuwepo na biashara ya uuzaji wa viungo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa mujibu wa ripoti ya mpasuaji wa maiti wa serikali, baadhi ya waathiriwa walifariki kutokana na ukosefu wa hewa, wengine walinyongwa wakati wengine wakifaa kutokana na makali ya njaa.
Taarifa hii ya wachunguzi wa mataifa inakuja wakati huu ambapo maofisa wa polisi katika taifa hilo la Afrika Mashariki wakitarajiwa kuchimba makaburi zaidi kutafuta miili ambayo huenda bado imezikiwa katika shamba hilo la Shakaholo linalohusishwa na mchungaji Paul Makenzie.
Paul Makenzie ambaye kwa sasa anashikiliwa na maofisa wa polisi nchini humo, anakabiliwa na mashtaka ya kuwaongoza wafuasi wake kufunga hadi kufa akiwapa matumaini kuwa kufanya hivyo ilikuwa njia ya kumuona Mungu kwa haraka.
Kwa sasa mhubiri huyo ambaye mafundisho yake yamekashifiwa vikali na viongozi wa kidini na raia nchini Kenya, yuko chini ya ulinzi makali wa polisi uchunguzi zaidi ukiendelea ikihofiwa kuwa huenda washirika wake bado wanagali katika msitu huo.
Haya yanajiri wakati huu shirika la Msalaba Mwekundu nchini humo likisema kuwa watu 360 wameripotiwa kutoweka, huku mamlaka ikisema wengine 60 wameokolewa wakiwa hai.
Tayari rais William Ruto ameunda tume ya uchunguzi kuchunguza vifo vya wafuasi wa dhehebu hilo akieeleza kuwa mhubiri huyo aliyemtaja kuwa gaidi anafaa kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Idadi ya vifo imefikia imepita 110, lakini inaweza kuongezeka zaidi, hii ni moja ya maafa makubwa sana yanayohusiana na imani za kidini katika historia ya hivi karibuni.
Waziri wa usalama wa ndani nchini Kenya , Kithure Kindiki amesema huenda kukawa na makaburi zaidi Shakahola huku akiwataka wanasiasa kutokaribia eneo hilo.
Wito wa waziri Kindiki umekuja baada ya kiongozi wa upinzani nchini humo Raila Odinga kuzuiliwa na walinda usalama wiki iliyopita wakati akitaka kuingia katika msitu huo.Odinga anadai kuwa kuna kitu ambacho serikali inaficha na ndio sababu za kuzuiliwa kwake.