Wapinzani wamtaka rais Saied ajiuzulu baada ya uchaguzi wa wabunge
Muungano wa upinzani nchini Tunisia, umemtaka rais Kais Saied kujiuzulu baada ya idadi ndogo ya wapiga kura kujitokeza kushiriki kwenye uchaguzi wa wabunge uliofanyika Jumamosi iliyopita.
Imechapishwa:
Kiongozi wa muungano huo Nejib Chebbi, amesema uchaguzi huo ni kichekesho na kuitisha maandamano, kushinikiza rais Saied kujiuzulu na kutaka uchaguzi wa urais kufanyika.
Tume ya uchaguzi inasema, ni chini ya asilimia 9 ya wapiga kura, ndio waliojitokeza kushiriki kwenye zoezi hilo.
Vyama vya upinzani, viliwaambia wafuasi wao, kususia uchaguzi huo, wakimshtumu rais Saied, kurudisha nyuma juhudi za demokrasia zilizopigwa nchini humo, tangu maandamano makubwa ya umma mwaka 2011.
Mzozo wa kisiasa ulianza kushuhudiwa tena katika taifa hilo la Afrika Kaskazini, baada ya rais Saied, mwenye umri wa miaka 64, kulivunja bunge na kubadilisha katiba mwaka huu, kwa kile anachosema nchi hiyo inahitaji kiongozi mwenye mamlaka makubwa ili kudhibiti hali ya kisiasa na rushwa nchini humo.