Vita Tigray: Mazungumzo ya amani yaliyopangwa nchini Afrika Kusini yaahirishwa
Mazungumzo ya amani yaliyokuwa yafanyike wikendi hii kati ya serikali ya Ethiopia na mamlaka ya Tigraya nchini Afrika Kusini yameahirishwa hadi tarehe nyingine. Hii imebainishwa na vyanzo viwili vya kidiplomasia vilivyonukuliwa na shirika la habari la Reuters siku ya Ijumaa.
Imechapishwa:
Ethiopia haikutoa maoni yoyote. Lakini chanzo cha Tigray kimeyaja "ukosefu wa maandalizi" na kulalamika kwamba mamlaka ya Mekele haikushauriwa kabla.
Juzi Jumatano Serikali ya Ethiopia ilikuwa ilisema, imekubali ombi la Umoja wa Afrika, kushiriki kwenye mazungumzo ya amani na waasi wa Tigray, kujaribu kumaliza mapigano ambayp yamekuwa yakiendelea kwa miaka miwili.
Redwan Hussein, mshauri wa masuala ya usalama kwa Waziri Mkuu Abiy Ahmed kupitia ukurasa wake wa Twitter, alithibitisha serikali kukubali ombi hilo akisema inaendana na msimamo wa serikali wa kutaka mzozo huo kutatuliwa kwa amani.
Jana Alhamisi kiongozi wa waasi wa Tigray alisema yuko tayari kutuma wajumbe kushiriki mazungumzo nchini Afrika Kusini lakini ataomba kujuwa mazungumzo hayo yatafanyika katika mazingira gani.
Kulingana na ripoti za kidiplomasia, mazungumzo hayo yangeliongozwa na mjumbe wa Umoja wa Afrika kwenye ukanda wa pembe ya Afrika, rais wa zamani wa Nigeria, Olusegun Obasanja na aliyekuwa rais wa Kenya Uhuru Kenyatta.