Rekodi ya ukame nchini Somalia, watu milioni moja watoroka makazi yao
Wasomali milioni moja wamelazimika kutoroka makazi yao kutokana na ukame wa kihistoria nchini humo. Ukame ambao umewaacha taabani watu zaidi ya milioni 7.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa na shirika linalohudumia Wakimbizi la Norway (NRC), watu 750,000 wametoroka makazi yao nchini humo tangu mwanzoni mwa mwaka huu kutokana na mabadiliko ya tabia nchi, na kufanya idadi ya watu waliotoroka makazi yao kufikia milioni 1 tangu mwezi Januari 2021, tarehe ambayo hali hii ya ukame ambao haujawahi kutokea ulianza.
Umoja wa Mataifa na shirika linalohudumia Wakimbizi la Norway (NRC) wanabaini kwamba familia zililazimika kutoroka makazi yao kwa sababu hakuna maji au chakula katika vijiji vyao. NRC inaomba "haraka" wafadhili kuongeza misaada "kabla hali haijawa mbaya zaidi".
Hadi kufikia mwezi Mei, kulingana na ripoti ya hivi karibuni kutoka ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA, Wasomali wapatao milioni 6.1 wameathiriwa na wako katika hali ya dharura kutokana na ukame.
Kati ya idadi hiyo, 771,400 wamelazimika kuyahama makazi yao kwa ajili ya kwenda kutafuta maji, chakula na malisho, wengi wao wakiwa wanawake na watoto.
Mtazamo umezidi kuwa mbaya kutokana na matarajio ya kutokuwa na msimu wa mvua unaopaswa kwa mwaka wa tano mfululizo.