Rais wa Ufaransa kufanya ziara Africa Magharibi
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron anatarajiwa kuzuru mataifa ya Cameroon ,Benin na Guinea Bissau wiki ijayo, ikiwa ni ziara yake ya kwanza barani Afrika baada ya kuchaguliwa tena kuongoza nchi yake kwa muhula wa pili.
Imechapishwa:
Ofisi ya rais jijini Paris imesema ,rais Macron atatumia ziara hiyo itakayoanzia nchi ya Cameroon kuanzia siku ya Jumatatu lengo kuu likiwa ni kuimarisha ushirikiano wa Ufaransa na bara la Afrika.
Cameroon imeendelea kushuhudia utovu wa usalama ambapo raia wameendelea kupoteza maisha katika mapigano kati ya vikosi vya serikali na waasi katika maeneo ya Kaskazini na Kusini Magharibi.
Maswala mengine muhimu yatakayopewa kipau mbele katika ziara hiyo ni pamoja na usalama wa chakula ambao umeathiriwa na vita vya Ukraine,kilimo na usalama .
Rais Macron juma lilopita alisema serikali yake inatathmini upya mpango wa ushirikiano wa kijeshi katika nchi zinazokabiliwa na makundi ya kijihadi baada ya kuondoa wanajeshi wake nchini Mali, baada ya kuzuka kwa mvutano kati ya uongozi wa kijeshi jijini Bamako na Paris.