Ripoti: Maafa makubwa yanaweza kuwakabili wagonjwa mahututi wa COVID Afrika
Wagonjwa mahututi wanaosumbuliwa na maambukizi ya COVID-19 barani Afrika, wapo kwenye hatari kubwa ya kupoteza maisha kwa sababu ya ukosefu wa vifaa muhimu vya kusaidia kutoa huduma za matibabu.
Imechapishwa:
Ripoti iliyotolewa na watalaam kutoka Hospitali ya Groote Schuur na Chuo Kikuu cha Cape Town nchini Afrika Kusini, imeeleza kuwa hii imethibitishwa kufuatia uchunguzi uliofanywa katika mataifa mbalimbali barani Afrika.
Aidha, imebainika kuwa mataifa ya Afrika yanapata changamoto za kutoa huduma nzuri kwa wagonjwa wa Covid 19 kwa sababu ya ukosefu wa vitanda, vyumba maalum lakini pia ukosefu wa fedha.
Nusu ya wagonjwa 3,000 waliokuwa mahututi waliolazwa hospitalini kati ya mwezi Mei na Disemba katika mataifa 10, walipoteza maisha.
Miongoni mwa mataifa yaliyofanyiwa utafiti ni pamoja na Misri, Ethiopia, Kenya, Libya, Msumbiji na mengine.
Ripoti hii imetolewa wakati huu bara la Afrika likiwa na maafa ya watu 130,000 tangu kuzuka kwa maambukizi hayo mwaka uliopita.