Libya: Vikosi vya Marshal Haftar vyataka kuendelea na mashambulizi
Vikosi vya Marshal Khalifa Haftar vimesema kuwa vinakusudia kuendelea na mashambulio yao dhidi ya vikosi vinavyounga mkono Serikali ya Tripoli inayoungwa mkono na jumuiya ya kimataifa.
Imechapishwa:
Vikosi hivyo vimefutilia mbali wito wa kusitisha mapigano uliyotolewa na marais wa Urusi na Uturuki.
Siku ya Jumatano Vladimir Putin na Recep Tayyip Erdogan walitoa wito wa kusitisha mapigano nchini Libya kuanzia usiku wa manane Januari 12 na kuwasihi mahasimu kutoka pande zote kuketi kwenye meza ya mazungumzo ili kufikia amani ya kudumu.
Katika taarifa, vikosi vya Marshal Khalifa Haftar (LNA) vimekaribisha pendekezo la Urusi kuhusu "amani na utulivu nchini Libya", lakini vimeonyesha nia yao ya kuendelea na "juhudi za vita yao dhidi ya makundi ya kigaidi (...) ambayo yanadhibiti mji mkuu wa Tripoli ".
Mwezi Aprili vikosi vya ANL, ambavyo vinadhibiti Mashariki mwa nchi, vilizindua mashambulio kuelekea magharibi mwa nchi na tangu wakati huo vinajaribu kuteka mji mkuu, Tripoli.