Rais wa Burkina Faso atetea umuhimu wa kikosi cha ukanda cha G5 Sahel
Siku kumi baada ya mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya kiuchumi ya Mataifa ya magharibi mwa Afrika uliofanyika jijini Ouagadougou, mkutano mwengine mpya wa viongozi wa mataifa ya Afrika magharibi unatarajiwa kufanyika hii leo Jumatano jijini New York kuzungumzia hali inayojiri nchini Mali na ukanda wa Sahel.
Imechapishwa:
Mbali na viongozi wa ukanda wa Afrika magharibi, wanatarajiwa pia kushiriki katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, rais wa tume ya Umoja wa Afrika, pamoja na mawaziri wa mambo ya nje wa Ufaransa na wa Algeria lakini pia muakilishi maalum wa Umoja wa Ulaya.
Akizungumza jana wakati wa kikao cha Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya tabia nchi kinachoendelea huko New York, nchini Marekani, Marc Christian Kabore mwenyekiti wa nchi za ukanda wa Sahel G5 Sahel, amebaini matumaini yake kuhusu maswala ambayo bado yanaendelea kuleta utata na kuzuia ufanisi wa vikosi vya usalama.
Mbali na hayo Marc Christian Kabore amesema chanzo cha kuyumba kwa usalama katika ukanda wa Sahel kunatokana na hali inayoendelea nchini Libya.