Pata taarifa kuu
SUDANI-SIASA-USALAMA-MAANDAMANO

Jeshi la Sudani lapewa muda wa miezi 3 kukabidhi madaraka kwa raia

Viongozi kutoka nchi kadhaa za Afrika waliokutana Jumanne wiki hii nchini Misri wametoa muda wa miezi mitatu kwa jeshi la Sudani kukabidhi madaraka kwa raia.

Rais wa Misri  Abdel Fattah al-Sissi, ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika.
Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sissi, ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika. AFP/Egyptian Presidency/Str
Matangazo ya kibiashara

Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sissi amesema muda wa miezi mitatu umetolewa kwa jeshi la Sudan kukabidhi madaraka kwa raia, akibaini kwamba uamuzi huo umechukuliwa bila kupingwa na viongozi walioshiriki mkutano wa Cairo Jumanne wiki hii.

Baadhi wamemshtumu rais wa Misri, ambaye ni Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika kuwa na ushirikiano wa karibu na viongozi wa jeshi waliompindua Omar al-Bashir.

Wengine wamekwenda mbali na kumuita Sissi kuwa ni dikteta na “anataka kusaidia jeshi kuendelea kushikilia madaraka kama anavyofanya yeye nchini mwake, ambapo aliingia madarakani kupitia jaribio la mapinduzi dhidi ya rais aliyechaguliwa Mohammed Morsi, na hivi amebadili katiba ili aendelea kusalia mamlakani”.

Uamuzi huo umekosolewa na waandamanaji ambao wanaendelea kupiga kambi mbele ya makao makuu ya jeshi jijini Khartoum.

Rais wa Misri amebaini kwamba mawaziri wa mambo ya nje kutoka nchi hizo zilizowakilishwa katika mkutano huo watakutana ndani ya mwezi mmoja ili kutathmini hali ya mambo nchini Sudani.

Rais wa Misri amesema washiriki katika mkutano huo waliomba jumuiya ya kimataifa kusaidia Sudan kiuchumi.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, rais Sissi alisisitiza haja ya kupata suluhisho la Kiafrika kwa mgogoro wa Sudan huku akitoa wito wa msaada wa kimataifa kwa uchumi wa Sudani.

Alielezea msimamo wa Misri kuunga mkono nia ya wananchi wa Sudan ili kufikia serikali ya kiraia.

Hata hivyo, alisema kuwa mabadiliko ya kidemokrasia yanahitaji muda wa kufikia uchaguzi huru na wa haki. Wakati huo huo alionya kuhusu kutokea hatari ya machafuko.

Awali Umoja wa Afrika ulitoa siku kumi na tano kwa jeshi kukabidhi madaraka kwa raia na hivyo kutoa vitisho kwa jeshi iwapo hawatofanya hivyo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.