Wahamiaji nane wafariki dunia kwa kukosa hewa
Wahamiaji nane wamepoteza maisha kwa kukosa hewa baada ya kukutwa ndani ya kontena lililoachwa mjini Zuwara, Magharibi mwa Libya.. Ripoti zinasema kuwa watu hao ni watoto sita, mwanamke mmoja pamoja na kijana mmoja ambao walikosa hewa.
Imechapishwa:
Chanzo cha polisi kinasema watu 8, ikiwa ni pamoja na watoto sita, walifariki dunia katika gari lenye kontena ambalo lilikuwa limebeba wahamiaji mia moja Jumatatu wiki hii karibu na mji wa Zuwara.
"Baada ya kufungwa kwa muda mrefu katika kontena, wahamiaji nane, ikiwa ni pamoja na watoto sita, mwanamke mmoja na mvulana mmoja, walikutwa wamefariki dunia kwa kukosa hewa," chanzo hicho kimesema katika taarifa iliyorushwa kwenye ukurasa wake wa Facebook.
"Tumepokea taarifakuhusu kuwepo kwa lori lenye kontena mashariki mwa Zouara)," amesema msemaji wa serikali ya eneo hilo, Hafed Mouammar. "Katika kontena hiyo tulikuta wahamiaji 100 kutoka nchi mbalimbali za Afrika na Asia (...) wakiwa katika hali ya uchovu mkubwa na wengi wakionekana wamekosa hewa".
Watu wenye shida ya kupumua walipokelewa katika vyumba vya uangalizi maalumu vya Idara ya Dharura ya Hospitali ya Zouara, mji wa pwani ulio kilomita 100 magharibi mwa Tripoli.
Kwa mujibu wa polisi, lori hilo lilikamatwa karibu na kampuni ya gesi ya Mellitah karibu na mpaka na Tunisia na karibu na mitambo ya bomba la gesi la Greenstream linalounganisha Libya na Italia.