Emmanuel Macron: Tunalaani uhalifu dhidi ya binadamu unaoendelea Libya
Ufaransa imelaani visa vya utumwa vinavyoendelea nchini Libya na kuomba mkutano wa dharura wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Imechapishwa:
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alitaja visa vya kuwauza wahamiaji kutoka Afrika kama watumwa Libya kuwa ni "uhalifu dhidi ya binadamu". Habari kuhusu visa vya kuwauza wahamiaji kama watumwa nchini Libya ilifichuliwa na kituo cha habari cha Marekani cha CNN.
"Hukumu ya Ufaransa haina rufaa" na "tunatakiwa kwenda mbali zaidi ili kuvunja mitandao" ya wafanyabiashara wa watu, aliongeza rais Macron baada ya kukutana katika ikulu ya Elysee na rais wa Guinea Alpha Condé, ambaye pia ni rais wa Umoja wa Afrika.
Wiki jana, kituo cha televisheni cha CNN kilifichua kuwepo kwa soko la watumwa karibu na mji wa Tripoli, hali ambayo ilishtumiwa katika Afrika na Ulaya.
Kwa mujibu wa rais Macron, "kilichofichuliwa" na CNN "ni wazi kwamba ni biashara ya binadamu. Ni uhalifu dhidi ya binadamu. Biashara hii haramu "ni uhalifu mkubwa zaidi" unaofanywa na "mitandao ya kigaidi". Biashara hii "inazalisha euro bilioni 30 kwa mwaka, kwa bahati mbaya inaathiri watu milioni 2.5 - na 80% ya waathirika ni wanawake na watoto," Rais Macron alisema.
Wakati huo huo, Ufaransa iliomba mkutano "wa dharura" wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ili kujadili kuuzwa kwa wahamaji hawa nchini Libya.