Tamasha la kuhimiza amani lamalizika Mashariki mwa DRC
Tamasha la Muziki lililopewa jina Amani, linamalizika mjini Goma Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Tamasha hili la kila mwaka, lilianza siku ya Ijumaa na lengo kuu ni kwa wanamuziki kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika, kutumia nyimbo zao kuwaleta watu pamoja ili kuhimiza amani Mashariki mwa nchi hiyo.
Waandalizi wa tamasha hili wanasema, wanaamini kuwa makundi ya waasi yamekuwa yakijisalimisha na kuacha kutekeleza mauaji dhidi ya raia kutokana na ujumbe unaotolewa kupitia kwa matamasha kama haya.
Mbali na wanamuziki, maafisa wa serikali ya DRC, Umoja wa Mataifa kupitia Mashirika ya UNESCO, UNICEF na wadau wengine pia wameshiriki katika tamasha hili kwa kuzungumza na makundi mbalimbali ya vijana kusaidia kufanikisha hili.
Kauli mbiu ya waandaji wa tamasha hili ambalo pia linafadhiliwa na kituo cha RFI na France 24, ni kuimba kwa ajili ya amani.
Mamia ya watu walijitokeza kushiriki katika tamasha hilo mjini Goma.
Mamia ya watu katika Jimbo la Kivu Kaskazini wamepoteza maisha baada ya kushambuliwa na waasi na wengine wameyakimbia makwao.