Mtandao wa Internet wazimwa nchini Gambia huku matokeo ya urais yakisubiriwa
Mtandao wa Internet umezimwa nchini Gambia wakati huu raia wa nchi hiyo wakisubiri matokeo ya Uchaguzi wa urais.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Raia wa nchi hiyo walipiga kura hapo jana kumchagua rais, na ushindani mkali unashuhudiwa kati ya rais Yahya Jammeh na mpinzani wake wa karibu Adama Barrow.
Hatua hii ya kuzimwa kwa Internet imekuja baada ya rais Jammeh ambaye ameongoza nchi hiyo kwa miaka 22, kuonya kuwa maandamano hayatakubaliwa baada ya matokeo ya mwisho kutangazwa.
Hatua hii imesababisha kuwa vigumu kwa wananchi wa taifa hilo kuwasiliana kupitia mitandao ya kijamii kama facebook na Twitter kama ilivyo kawaida.
Wapiga kura wapatao 880,000 walisajiliwa kupiga kura katika vituo 1400 nchini humo.
Waangalizi wa Kimataifa kutoka Umoja wa Ulaya hawakupewa vibali vya kuja kushuhudia uchaguzi huo.
Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kutangazwa mwishoni mwa wiki hii.