Sudan Kusini yailaumu DRC kuwaficha waasi
Juma moja baada ya aliyekuwa makamu wa rais wa Sudan Kusini Dr Riek Machar kuripotiwa kuwa yuko mjini Khartoum, nchini Sudan akipatiwa matibabu akitokea nchini DRC, utawala wa Juba, umeikosoa serikali ya Kinshasa kwa kuruhusu ardhi yake kutumiwa na waasi wa Machar.
Imechapishwa:
Akizungumza na wanahabari jijini Juba, Waziri wa habari na utangazaji nchini Sudan Kusini, Michael Makuei Lueth, amebainisha kitendo cha Machar kuruhusiwa kuingia nchini humo akitumia ndege za DRC kupitia ubalozi wake ni kinyume cha sheria za kimataifa, ambapo umemuagiza balozi wa DRC mjini Juba kutoa maelezo juu ya kitendo hicho.
Makuei amesema kuwa kitendo kilichofanywa na serikali ya Kinshasa, hakikubaliki na kwamba hakinufaishi upande wowote wa nchi kwa mustakabali wa amani ya ukanda na dunia.
Matamshi yake yamekuja baada ya kukutana na balozi wa DRC mjini Juba, na kumueleza kinaga ubaga kutoridhishwa kwake na uamuzi wa serikali ya Kinshasa, kumruhusu Machar na jeshi lake kuingia bila masharti au zuio.
Riek Machar alikimbia mjini Juba baada ya makazi yake kushambuliwa, kufuatia makabiliano kati ya vikosi vyake na vile vya Serikali, ambapo zaidi ya askari 200 kutoka kila upande waliuawa kwenye mapigano ya mwezi uliopita.