Pata taarifa kuu
TUNISIA-SHAMBULIZI-USALAMA

Tunisia yarefusha muda wa hali ya tahadhari kwa kipindi cha miezi miwili

Jumanne wiki hii, Ofisi ya rais wa Tunisia imetangaza kurefusha kwa kipindi cha miezi miwili muda wa hali ya tahadhari, uliyowekwa nchini kote baada ya shambulio la kujitoa mhanga la Novemba 24 dhidi ya basi la kikosi cha askari wa usalama wa rais na, ambalo liliwaua watu 12.

Rais wa Tunisia Beji Caid Essebsi, Novemba 25, 2015, Tunis.
Rais wa Tunisia Beji Caid Essebsi, Novemba 25, 2015, Tunis. AFP/AFP/
Matangazo ya kibiashara

Rais "Beji Caid Essebsi ameamua kurefusha muda wa hali ya tahadhari nchini kote kwa kipindi cha miezi miwili" au "mpaka Februari 21, 2016", Ofisi ya rais imesema katika taarifa yake. Hatua hii ya kipekee ingelitamatika Jumatano hii desemba 23, sawa na siku 30 baada ya kuanza kutekelezwa.

Hatua hii inawaruhusu viongozi kupiga marufuku migomo na mikutano "yenye lengo la kusababisha au kuzua machafuko", kufunga kwa muda " kumbi za sherehe na baa" pamoja na "kuchukua hatua zote ili kuhakikisha udhibiti wa vyombo vya habari na mashirika ya habari ya aina yoyote".

Katika mazingira ya shambulio la tarehe 24 Novemba, shambulio lililodaiwa kutekelezwa na kundi la Islamic State (IS), serikali pia ilitangaza amri ya kutotoka nje katika mji wa Grand Tunis, hatua ambayo ilifutwa, hata hivyo, siku kumi zilizopita.

Vikosi vya usalama vimeendelea na operesheni ya msako na kuwakamata baadhi ya watu wanaoshukiwa kutekeleza makosa mbalimbali, kwa mujibu wa mashirika yasio ya kiserikali, tangu kutokea kwa shambulio hilo jipya lililosababisha maafa katika mji wa Tunis.

Tunisia, ambayo ni mfano wa kuigwa kwa kipindi cha mpito katika mfumo wa kidemokrasia, inakabiliwa tangu mwaka 2011 na mashambulizi ya makundi ya wanamgambo wa kiislamu, ambayo yameua askari polisi na wanajeshi kadhaa pamoja na raia wa kawaida.

Kwa mujibu wa takwimu za serikali, Tunisia ni moja ya nchi ambayo ina raia wengi, karibu 6.000 katika safu ya makundi ya wanamgambo wa kiislamu nchini Syria, Iraq na nchi jirani ya Libya.

Kabla ya shambulio la kujitoa mhanga dhidi ya askari wa kikosi cha usalama wa rais Novemba 24, mashambulizi mengine makubwa mawili yalidaiwa kutekelezwa na kundi la kigaidi mwaka 2015, katika makavazi ya Bardo mwezi Machi ambayo yaliwaua watu 22, na shambulio jingine dhidi ya hoteli ya Sousse mwishoni mwa mwezi Juni, shambulio ambalo liliwaua watu 38.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.