Utekaji nyara wa raia wa Ufaransa wakithiri Madagascar
Kwa ushirikiano na viongozi wa Madagascar, ubalozi wa Ufaransa nchini Madagascar unataka kukomesha visa vya utekaji nyara kwa raia wake ambavyo vimekithiri nchini humo.
Imechapishwa:
Ubalozi wa Ufaransa nchini Madagascar umethibitisha kuwa na nia ya kuchukua hatua za kukomesha visa hivyo.
Nchini Madagascar, jamii ya raia wa Ufaransa inakabiliwa na visa vya utekaji nyara kuliko jamii zingine ziishio nchini humo. Raia wa Ufaransa kati ya 20 na 30 wamekua wakitekwa nyara kila mwaka, na idadi hiyo huenda ikaongezeka.
Tukio la hivi karibuni, juma moja lililopita, ni la kijana mmoja ambaye alitekwa nyara mbele ya shule anakosomea katika mji wa Tuléar. Kijana huyo ni kutoka jamii ya Karana ( jamii ya Waislamu inayoundwa na wahamiaji kutoka India na Pakistan), ambayo inalengwa kwa visa hivyo vya utekaji nyara. Kijana huyo aliachiliwa huru Ijumaa juma lililopita baada ya kutolewa fidia ya Yuro 11,000. Watu tisa wamekamatwa. Lakini Ufaransa umebaini kwamba “ visa hivyo vimekithiri”.
Kwa mujibu wa balozi wa Ufaransa nchini Madagascar, François Goldblatt, kushambulia kijana mdogo, ni jambo ambalo linatia huzuni. Kwa kukomesha visa vya utekaji nyara nchini Madagascar, François Goldblatt, amependekeza msaada wa vikosi vya Ufaransa kwa viongozi wa Madagascar.