Mugabe yaweza kusafiri Ulaya
Umoja wa Ulaya umesema uko tayari kuondoa kwa muda vikwazo vinavyomkabili rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe, ambaye amepigwa marufuku kusafiri kwenda kwenye Umoja huo ikiwa atazuru Mataifa hayo kama mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, AU.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kauli hiyo imetolewa na msemaji wa Idara ya Kidiplomasia ya Umoja huo Bi. Catherine Ray katika mkutano na waandishi wa habari jijini Brussels nchini Ubelgiji.
Tangu mwaka 2013, Umoja wa Ulaya umekuwa ukirejesha mahusiano yake na nchi ya Zimbabwe, kwa kuondoa baadhi ya vikwazo vya kiuchumi ilivyoiwekea mwaka 2002, kupinga ghasia za kisiasa na ukiukaji wa haki za binadamu ambao ulidaiwa kufanywa na serikali ya Mugabe.
Rais Mugabe na mkewe, Grace Mugabe, wako kwenye orodha ya watu waliopigwa marufuku kupewa viza ya kuingia Ulaya ambapo mwezi Aprili mwaka uliopita rais huyo aligoma kwenda kwenye mkutano baina ya Ulaya na Afrika mjini Brussels kwa mwaliko maalum kwa sababu ya kumnyima viza mke wake.
Hata hivyo, rais Mugabe hatapata fursa ya kusafiri kuelekea mjini Brussels kwa kipindi cha wenyekiti wake wa Umoja wa Afrika kwa vile hakuna mkutano wowote ulioandaliwa baina ya Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika kwa mwaka 2015.