Jammeh awateua wanahabari katika serikali yake
Wiki moja baada ya jaribio la kumwondoa madarakani, rais wa Gambia Yahya Jammeh, kiongozi huyo amewateua wanabahari wawili katika Baraza lake la Mawaziri.
Imechapishwa:
Sherri Bojang mwandishi wa Habari wa Gazeti la The Standard ameteuliwa kuwa Waziri wa habari na mawasiliano huku eneh Macdouall-Gaye, akiteuliwa kuwa Waziri wa mambo ya nje.
Hakuna sababu yoyote iliyotolewa na Ikulu ya Banjul kuhusu mabadiliko hayo ya ghafla.
Rais Jammeh ameyashtumu mataifa ya magharibi kwa kuchochea jaribio la kutaka kumwondoa madarakani, na tayari Marekani imewafungulia mashtaka watu wawili wanaotuhumiwa kuhusika katika mpango huo.
Rais Yahya Jammeh ametangaza pia kuwa atatoa mfano kwa watu wengine wenye kuwa na nia ya kuyumbisha usalama katika nchi hiyo.
Hii imekuja baada ya kunaswa kwa wanajeshi kufanya jaribio la mapinduzi mwishoni mwa mwaka uliopita, wakati akiwa mapumzikoni Dubai.
Akizungumza mbele ya wafuasi wake waliokuja kumuunga mkono jijini Banjul, rais Jammeh amesema anataka kuondokana na waasi mmoja hadi mwingine.
Kauli hii ya rais Jammeh imezua hofu miongoni mwa wanaharakati wa haki za binadamu ambao wanaona huenda watu hao wakanyongwa.