Serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati yatangaza kusitisha huduma ya SMS
Huduma ya ujumbe mfupi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati hivi sasa imeonekana kuwa tishio la usalama kwenye taifa hilo ambapo Serikali ya nchi hiyo sasa imetangaza kuzuia kwa muda huduma hiyo.
Imechapishwa:
Hatua hiyo imechukuliwa baada ya kuwepo kwa dalili kuwa unachangia kuhamasisha machafuko nchini humo.
Hatua hiyo ya kiusalama imetangazwa jana na Wizara ya Posta na Mawasiliano na kuanza kutekelezwa hadi itakapotangazwa tena upya ili kuchangia kurejesha usalama katika nchi ambayo imegubikwa na matukio ya vurugu na ukiukwaji wa haki za binadamu.
Uamuzi huo unakuja baada ya Waziri mkuu wa nchi hiyo André NZAPAYEKE kuwaandikia barua Waziri na wakurugenzi wa Posta na mawasiliano baada ya vurugu zilizojitokeza juma lililopita na baada ya wito wa mgomo uliotolewa mapema wiki hii kwa njia ya sms.
Aidha, hatua hii inakuja baada ya wito wa Waziri mkuu kuwaomba wafanyakazi wote warejee kazini kuanzia jana baada ya siku kadhaa za maandamano na kusimamishwa kwa shughuli zote za kijamii mjini Bangui.
Taarifa kutoka vyanzo vya kiserikali zimebaini kuwa matumizi ya ujumbe mfupi au sms yatasimamishwa kwa siku chache zijazo, na tayari watu wakijaribu kutuma ujumbe wa maandishi kupitia mtandao wa Orange maarufu mjini Bangui yanatokea majibu kwamba ni marufuku kuandika SMS.