Rais wa Sudan, Omar al-Bashir atangaza mabadiliko makubwa katika serikali yake
Rais wa Sudan Omar al-Bashir amewatangaza makamu wake wawili wa Rais na kulitaja baraza jipya la Mawaziri, katika mabadiliko makubwa kuwahi kufanywa na chama tawala cha National Congress Party NCP, ambacho kimekuwa kikikosolewa utawala wake usiokubali mabadiliko kwa zaidi ya miongo miwili.
Imechapishwa:
Bakri Hassan Saleh ametangazwa kuwa makamu wa kwanza wa Rais akichukua nafasi ya Ali Osman Taha ambaye alijiuzulu ili kupisha uundwaji wa serikali mpya.
Saleh ni miongoni mwa vinara wa mapinduzi ya mwaka 1989 yaliyomuweka madarakani Rais al Bashir.
Aliyekuwa katibu wa siasa wa chama hicho, Hassabo Mohammed Abdel Rahman ametangazwa kuwa makamu wa pili wa Rais.
Mabadiliko hayo yanatafsiriwa kama ishara ya kuwatuliza wananchi ambao hivi karibuni waliandamana kupinga hatua ya serikali kuondoa ruzuku ya mafuta na kupanda kwa gharama za maisha.
Katika mabadiliko hayo Rais Bashir amewataja Mawaziri wapya wasiopungua watano kutoka vijana wa chama tawala cha NCP.