Mkutano wa Pili kuhusu Amani wafunguliwa Paris
Viongozi mbalimbali wa dunia wanakutana jijini Paris nchini Ufaransa, kujadili masuala kuhusu mabadliko ya hali ya hewa, usalama na uongozi bora.
Imechapishwa:
Rais wa Ufaransa Emmaniuel Macron, anatumia fursa hii kuonyesha nafasi ya nchi yake, katika kufanikisha jitihada za mabadiliko ya hali ya hewa na kuyakumbusha mataifa ya dunia kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mkataba wa Paris mwaka 2015.
Mkutano huo ambao unafayika Kaskazini mwa mji mkuu wa Ufaransa utadumu siku mbili kuanzia leo Jumanne.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ambaye alitoa hotuba ya utangulizi Jumatatu wiki hii, aliwataka washiriki wa mkutano huo kutazama jinsi ya kutafutia ufumbuzi hali inayoikumba dunia leo, akisema, kwa sasa dunia inatia huzuni kwa "yale yanayoikabili"
Antonio Guterres amesema ushirikiano kati ya nchi, kati ya mashirika mbalimbali na wanaharakati mbalimbali ndio suluhu pekee katika matatizo yanayoikabili dunia kwa sasa.
Hii ni mara ya pili Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatoa ujumbe kama huo. Alifanya hivyo mwaka jana, katika mkutano wa kwanza wa amani, katika maadhimisho ya ya miaka 100 kumalizika kwa Vita vya Kwanza vya Dunia.