Brexit: Umoja wa Ulaya na Uingereza waendelea na mazungumzo
Serikali ya Uingereza inasema mazungumzo bado yanaendelea kati yake na viongozi wa Umoja wa Ulaya, kuhusu uwezekano wa kupatikana kwa mkataba mpya wa namna nchi hiyo itakavyojiondoa kwenye Umoja huo.
Imechapishwa:
Waziri Mkuu Boris Johnson anaendelea kupata shinikizo za kupata mkataba mpya kufikia Alhamisi wiki hii, siku ambayo kutakuwa na mkutano mkuu wa viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya.
Hivi karibuni Waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson aliahidi kuifanya Uingereza kuwa nchi ya neema kuliko nchi yoyote duniani na alisisitiza msimamo wake wa kwamba nchi hiyo itatoka kwenye Umoja wa Ulaya.
Waziri Mkuu Boris Johnson alisema jukumu la serikali yake ni kuiondoa Uingereza kutoka Umoja wa Ulaya tarehe 31 mwezi Oktoba ili kuwaleta Waingereza wote pamoja na kuiimarisha nchi.
Waziri Mkuu huyo mpya aliahidi kufikia mapatano mapya na Umoja wa Ulaya katika muda usiozidi siku 99 lakini alionya kwamba, ikiwa viongozi wa Umoja wa Ulaya watakataa, basi Uingereza itajiondoa bila ya mkataba. Hata hivyo alibaini kwamba masharti yaliyomo kwenye mkataba wa sasa hayakubaliki.