Waziri Mkuu nchini Uingereza kumwomba Malkia kusitisha bunge
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson anatarajiwa kumwomba Malkia kusitisha shughuli za bunge katikati ya mwezi Septemba.
Imechapishwa:
Hii inamaana kuwa wabunge hawatakuwa na nafasi ya kuzuia nchi hiyo kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya ifikapo mwisho wa mwezi Oktoba bila ya mkataba kama ambavyo wamekuwa wakipanga, iwapo ombi la Waziri Mkuu litakubaliwa.
Tayari Waziri Mkuu Johnson, amesema ni lazima Uingereza ijiondoe kwenye Umoja huo ikiwa na mkataba au bila mkataba huo ifikapo tarehe 31 mwezi Oktoba.
Ripoti zinasema kuwa, wabunge hawatakuwa kazini, kati ya tarehe 9 mwezi Septemba hadi tarehe 14 mwezi Oktoba siku ambayo Malkia Elizabeth wa pili, atakapotoa hotuba kwa bunge.
Ofisi ya Waziri Mkuu inasema hatua hiyo itamsaidia Johnson kushughulikia kikamilifu masuala ya ndani ya nchi hiyo kama uhalifu na elimu.
Hata hivyo, hatua hiyo imeelezwa na serikali kama nafasi kwa wabunge kujadili kwa kirefu kujiondoa kwenye Umoja huo kuelekea mkutano wa viongozi wa Umoja wa Ulaya tarehe 17 mwezi Oktoba.
Wabunge wa upinzani wamelaani hatua hii na kusema, kuwa Waziri Mkuu Johnson anataka kulazimisha Uingereza kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya hata bila mkataba.