Wakuu wa Umoja wa Ulaya watoa onyo kwa atakayekuwa Waziri Mkuu mpya wa Uingereza
Viongozi wa Umoja wa Ulaya, wametoa onyo kwa Waziri Mkuu ajaye wa Uingereza, asitegemee mabadiliko yoyote kwenye mkataba ulioafikiwa kuhusu nchi hiyo kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya.
Imechapishwa:
Onyo hili limekuja wakati aliyekuwa Waziri wa Mambo ya nje Boris Johnson akitarajiwa kumenyena na Waziri wa Mambo ya nje wa sasa Jeremy Hunt, kuongoza chama cha Conservative na baadaye Waziri Mkuu mpya.
Wawili hao wameweka wazi kuwa wanataka majadiliano mapya na Umoja wa Ulaya kuhusu mkataba huo wa kujiondoa, ambao viongozi wa Umoja wa Ulaya, walikuwa wamekubaliana na Waziri Mkuu anayeondoka Theresa May.
Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya Donald Tusk amesema, Umoja huo hautabadilisha mkataba huo lakini, utaivumilia Uingereza katika mchakato wa kujiondoa.
Kuelekea Oktoba tarehe 31, siku ya mwisho ya Uingereza kujiondoa kwenye Umoja huo, Tusk amesema kuwa viongozi wa EU wako tayari kufanya kazi na yeyote atakayekuwa Waziri Mkuu mpya wa Uingereza.