Wiki muhimu kwa Uingereza kujitoa EU yawadia
Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May anatarajia kukutana na serikali yake leo Jumatatu wakati wiki hii ni muhimu kwa Uingereza katika mpango wake wa kujitoa katika Umoja wa Ulaya.
Imechapishwa:
Hata hivyo Theresa May anakabiliwa na kazi kubwa ya kufikia ndoto yake wakati Bunge la Uingereza limeendelea kutilia mashaka mchakato wa Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya, huku Waziri Mkuu akiwa mashakani kupoteza imani ya wabunge.
Wiki hii pia ni muhimu kwa wafuasi wa Brexit, ambapo Ijumaa, Machi 29, saa 23:00 sa za kimataifa, Uingereza ingeweza kuwa imejitoa katika Umoja wa Ulaya, miaka mitatu baada ya kura ya maoni ya Juni 23, 2016.
Lakini baada ya kushindwa kukinaisha wabunge wa Uingereza kuunga mkono makubaliano ya Uingereza kujitoa katika umoja huo yaliyofikiwa baada ya mazungumzo na Brussels, Theresa May alilazimika kuomba viongozi wa Umoja wa Ulaya kusogeza mbele tarehe hiyo ya kihistoria hadi Aprili 12, tarehe ambayo hata hivyo inatarajiwa kupitishwa na Bunge.