Mtuhumiwa wa mauaji ya Strasbourg auawa na polisi
Mtuhumiwa ambaye aliwaua watu watatu katika soko moja la Christmas mjini Strasbourg, Ufaransa, ameuawa kwa kupigwa risasi na vyombo vya usalama wakati huu kundi la Islamic State likidai kuwa mtu huyo alikuwa mpiganaji wake.
Imechapishwa:
Kuuawa kwake kumekuja baada ya Serikali kusambaza zaidi ya askari 700 kumsaka Cherif Chekatt, mwenye umri wa miaka 29, ambaye alikimbia tangu alipotekeleza shambulio hilo Jumanne ya wiki hii.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ufaransa Christophe Castaner amesema polisi watatu walijaribu kumuhoji Chekatt baada ya kumbaini kwenye mtaa mmoja kaskazini mwa mjini wa Neudorf ambako alikulia, lakini aliwafyatulia risasi hali iliyowafanya polisi nao kujibu.
Kwa mujibu wa vyanzo vya karibu na idara ya polisi nchini Ufaransa, vimedai kuwa Chekatt aligunduliwa na mwanamke mmoja aliyetambua sura yake pamoja na jeraha la mkono alilokuwa nalo baada ya kujeruhiwa wakati wa makabiliano na vyombo vya usalama siku ya Jumanne.
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameendelea kusisitiza Serikali yake kukabiliana na matukio kama haya wakati huu soko hilo likitarajiwa kufunguliwa tena kwa mara nyingine leo Ijumaa.