Aquarius yaruhusiwa kutia nanga Malta, wahamiaji kutawanywa katika nchi tano za Ulaya
Meli ya Aquarius ya shirika la kihisani inayobeba wahamiaji 141 ambayo ilikua imekwama katika bahari ya Mediterania imeruhusiwa kutia nanga katika bandari ya Malta. Ufaransa imepongeza viongozi wa Malta kwa hatua hiyo.
Imechapishwa:
Uhispania imekubali kupokea wahamiaji 60 kutoka Aquarius, wengine watatawanywa kati ya Ufaransa (ambayo imekubali kupokea wahamiaji 60, kulingana taarifa ya ikulu ya Elysee), Ujerumani, Luxemburg au Ureno, ambayo imesema iko "tayari" kupokea wahamiaji 30. Wengi wa wahamiaji hao ni kutoka Eritrea na Somalia.
Kuruhusiwa kwa meli hiyo kumetokana na makubaliano ya hivi karibuni yaliyosainiwa kati ya nchi kadhaa za Ulaya na kutamatisha siku nne za mgogoro mpya kuhusu hatima ya wahamiaji waliookolewa na meli hiyo ya Aquarius. Italia, Uspania na Tunisia walikataa meli hiyo kutia nanga katika moja ya bandari zao.
Siku ya Ijumaa, Aquarius, iliyokodiwa na shirika la kihisani la SOS Mediterranean na shirika la Madaktari Wasio na Mipaka (MSF), iliwaokoa watu 141 kutoka Libya, ambao walikuwa katika boti mbili zilizotengenezwa kwa mbao, ambapo nusu ya wahamiaji hao ni watoto na zaidi ya theluthi moja ni wanawake.
Kwenye ukurasa wake wa Twitter, rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amekaribisha hatua ya serikali ya Malta ya kuruhusu meli ya Aquarius kutia nanga katika bandari yake.
Concrete European cooperation enacted on the #Aquarius, based on a French-Maltese initiative. I thank Malta for its humanitarian gesture and assure it of the full solidarity of France. There is no alternative to cooperation. https://t.co/OXaO2SRZgm
Emmanuel Macron (@EmmanuelMacron) August 14, 2018
Suluhisho limepatikana kupitia mazungumzo kati ya Ufaransa na Malta, kwa msaada wa Tume ya Ulaya. Ilichukua siku nne tu kwa Umoja wa Ulaya ili kuondokana na mgogoro huu mpya unaohusiana na wahamiaji, mwandishi wetu huko Brussels, Laxmi Lota, amearifu.