Mawaziri wa fedha kutoka nchi za G20 waikashifu Marekani
Nchi ya Marekani imesema haitaki vita ya kibiashara kutokana na tangazo lake kuhusu kodi mpya za forodha lakini ikasisitiza kuwa haitamuogopa mtu, haya ni matamshi ya waziri wa fedha wa Marekani Steven Mnuchin baada ya mkutano wake na mawaziri wa fedha kutoka nchi za G20.
Imechapishwa:
Vita ya kibiashara sio lengo letu lakini hatuiogopi alisema Mnuchin wakati wa kuhitimishwa kwa mkutano wa siku mbili wa mawaziri wa fedha kutoka nchi za G20 waliokutana mjini Buenos Aires Argentina.
Matamshi ya Mnuchin anayatoa wakati huu nchi yake ikikosolewa kutokana na kutangaza kutoza ushuru wa forodha kwa bidhaa za Chuma na Aluminium zinazotoka nje ya Marekani.
"lazima tujiandae kuchukua hatua kwa manufaa ya Marekani katika kulinda uhuru na usawa wa biashara. katika kufanya hivi mara zote kuna hatari," alisema Mnuchin.
Mnuchini alikuwa akizungumza baada ya mawaziri hao wa fedha kukubaliana kulaani hatua ya Marekani.
Taarifa ya pamoja ya mawaziri hawa imetolewa ikiwa ni siku moja tu imebaki kabla ya kuanza kutumika rasmi kwa sheria iliyotiwa saini na rais Trump kuhuus ushuru wa forodha kwa bidhaa za nje.
Mawaziri hao wamesema kuwa hatua ya Marekani haina lengo jema katika ushirikiano wa kibiashara kati ya nchi wanachama, na kwamba kodi iliyotangazwa kutozwa na Marekani itaathiri biashara baina ya mataifa yao.
Wakati akitia saini mkataba huo rais Trump alisema lengo sio kuzikomoa nchi zinazofanya biashara na Marekani lakini imelenga katika kuimarisha viwanda vyake vya ndani na kuzuia bidhaa zisizo na ubora kuingia nchini Marekani.
Nchi ya Canada na China zimekuwa nchi za awali kukashifu hatua ya Marekani kwa kuwa zimekuwa zikifanya biashara kubwa ya Chuma na Aluminium kwa taifa la Marekani.