Brexit: EU na Uingereza zafikia makubaliano kuhusu muda wa mpito
Nchi ya Uingereza na umoja wa Ulaya Jumatatu ya wiki hii wamefikia makubaliano muhimu kuhusu mchakato wa mpito ambao utadumu kwa muda wa miaka mwili baada ya nchi hiyo kujitoa kwenye umoja wa Ulaya hapo mwakani, amesema kiongozi wa ujumbe wa EU kwenye mazungumzo hayo Michel Barnier.
Imechapishwa:
Barnier amesema kuwa wamefikia makubaliano kuhusu muda wa mpito kwa nchi ya Uingereza kujitoa wakati alipozungumza na wanahabari jijini Brussels Ubelgiji baada ya kukutana na mwenzake wa Uingereza David Davis.
Taarifa mpya iliyotolewa na pande hizo mbili imeonesha kuwa makubaliano ya sasa yanatoa muda wa miaka miwili kuanzia pale Uingereza itakapokuwa imejitoa Machi 29, 2019 hadi Desemba 31, 2020.
Barnier ameongeza kuwa wakati wa kipindi hicho, nchi ya Uingereza haitashiriki kwenye vikao vya maamuzi vya umoja wa Ulaya kwa sababu baada ya siku hiyo gaitakuwa tena mwanachama.
Kwenye taarifa yake Barnier anasema Uingereza itaendelea kupata manufaa ikiwemo faida za soko la pamoja na ushuru wa forodha na kwamba italazmika kufuata sheria zote za umoja huo kama wanachama wengine.
Kwa upande wake Davis amesema kuwa muda wa mpito unatoa fursa ya kibiashara inayohitajika kwa nchi yake pamoja na raia wengine wa Uingereza na wale kutoka kwenye umoja wa Ulaya.
Makubaliano haya yamefikiwa baada ya miezi kadhaa ya mvutano kuhusu muda wa mpito ambao Uingereza inastahili kupewa baada ya kuwa imejitoa rasmi kwenye umoja huo.
Miongoni mwa masuala tata yaliyokuwa yakileta sintofahamu kuhusu makubaliano ya muda wa mpito ni pamoja na namna Uingereza itakavyofanya biashara kwenye umoja wa Ulaya baada ya kujitoa pamoja na haki za raia wengine kutoka umoja wa Ulaya kufanya kazi Uingereza.