Pata taarifa kuu
UFARANSA

Emmanuel Macron aapishwa rasmi asema yeye ni rais wa wote

Emmanuel Macron ameapishwa rasmi kuwa rais wa taifa la Ufaransa akichukua nafasi ya Francois Hollande aliyemaliza muda wake baada ya uchaguzi wa juma moja lililopita ulioshuhudia kuanguka kwa vyama vya Republican na Socialist.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron akihutubia baada ya kuapishwa. Mei 14, 2017
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron akihutubia baada ya kuapishwa. Mei 14, 2017 REUTERS/Francois Mori/Pool
Matangazo ya kibiashara

Macron sasa anakuwa rais kijana zaidi kushika nafasi ya urais kwenye taifa la Ufaransa na kuweka historia ya kuwa rais aliyechaguliwa kupitia vuguvugu la kisiasa na sio kutoka kwenye chama.

Macron aliwania urais kupitia vuguvugu la En Marche ambalo sasa limebadilishwa jina na kuitwa “la Republique en Marche”.

Akihutubia kwa mara ya kwanza kwenye ikulu ya Elysee akiwa kama rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron ameendelea kusisitiza umihimu wa wananchi wa Ufaransa kuungana na kuwa wa moja.

Rais mpya wa Ufaransa Emmanuel Macron (kulia) akipunga mkono kumuaga Hollande akiwa na mkewe Brigitte Trogneux kwenye ikulu ya Elysee. Mei 14, 2017
Rais mpya wa Ufaransa Emmanuel Macron (kulia) akipunga mkono kumuaga Hollande akiwa na mkewe Brigitte Trogneux kwenye ikulu ya Elysee. Mei 14, 2017 REUTERS/Christian Hartmann

“Huu ni muda wa wafaransa kuungana na kuweka kando tofauti zetu za kisiasa, hatupaswi kuangalia mimi au wewe tunatoka mrengo gani wa chama, mimi ni rais wa wote, ni rais wa wafaransa”. Alisema Macron kwenye hotuba yake.

Rais Macron amesema wananchi wa Ufaransa wamechagua tumaini na sasa wanatazama zaidi mustakabali wao wa baadae.

Kuhusu umoja wa Ulaya rais Macron amesema kuwa “Umoja wa Ulaya utabadilika na utazinduliwa upya” kauli anayotoa wakati huu ambapo siku ya Jumatatu ya Machi 15 anatarajiwa kuwa na mazungumzo na kansela wa Ujerimani, Angela Merkel.

Rais Francois Hollande akiondoka kwenye ikulu ya Elysee mara baadaya kukabidhi madaraka kwa rais mpya Emmanuel Macron, Mei 14, 2016
Rais Francois Hollande akiondoka kwenye ikulu ya Elysee mara baadaya kukabidhi madaraka kwa rais mpya Emmanuel Macron, Mei 14, 2016 REUTERS/Yoan Valat/Pool

Wakati wa kampeni zake za kuingia ikulu, rais Macron alikuwa akisisitiza kuwa jukumu lake la kwanza kama rais wa Ufaransa ni kuhakikisha umoja wa Ulaya unabadilika na kufanyiwa mabadiliko makubwa ili kutoa fursa zaidi kwa mataifa kuondoa ushindano usio sawa na viwanda vya uchina lakini pia kwenye soko la ajira.

Macron anakuwa rais wa 8 wa jamhuri ya Ufaransa huku akiwa na umri wa miaka 39, akiwa ameachwa kwa zaidi ya miaka ishirini na mtangulizi wake Francois Hollande.

Kama ilivyo utamaduni wa taifa la Ufaransa, rais anayeondoka madarakani humpisha kwenye ikulu rais anayeingia ambapo punde baada ya makabidhiano, Hollande aliondoka kwenye ikulu ya Elysee akisindikizwa na mwenyeji wake Emmanuel Macron ambaye alimshuhudia akipanda gari kuondoka.

Rais Macron anaingia madarakani huku akitarajiwa kukabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo suala la ukosefu wa ajira, vita dhidi ya makundi ya kijihadi, mabadiliko kwenye umoja wa Ulaya, mdororo wa uchumi na kuwaunganisha wafaransa waliogawanyika baada ya uchaguzi mkuu wa Mei 7 mwaka huu.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.