Obama na Waziri Mkuu wa Ireland wamuunga mkono Emmanuel Macron
Rais wa zamani wa Marekani Barrack Obama na Waziri Mkuu wa Ireland Enda Kenny wamejitokeza wazi na kutangaza kumuunga mkono mgombea urais nchini Ufaransa Emmanuel Macron .
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wawili hao wamesema Macron ndiye mgombea mwenye sera za kuwaunganisha raia wa Ufaransa na watu wengine wa duniani kinyume na mpinzani wake Marine Le Pen.
Obama amesema mafanikio ya Ufaransa ni muhimu kwa dunia nzima na Macron ndiye anayeonekana kubeba maono hayo kuelekea duru ya pili ya Uchaguzi wa urais siku ya Jumapili.
“Nimekuwa nikifuatilia kwa karibu kampeni za Macron na hakika nimeridhika kuwa yeye ndiye anayesimamia mambo tunayoyaamini na ningependa kila mmoja afahamu kuwa namuunga mkono,” alisema Obama.
Wakati uo huo, Macron amemfungulia mashitaka mpinzani wake Le Pen baada ya kudai kuwa ana akaunti ya fedha katika nchi ya Bahamas, madai ambayo amesema ni ya kumharibia jina.
Kampeni zinaingia siku ya mwisho siku ya Ijumaa, huku wagombea hawa wakitumia siku hii ya mwisho kuwaomba raia wa nchi hiyo kuwapigia kura.
Siku ya Jumamosi, hakutakuwa na shughuli zozote za kisiasa au kampeni nchini humo huku kila mmoja akisubiri siku ya kupiga kura.
Kura za maoni zimekuwa zikionesha kuwa Macron ana nafasi kubwa ya kuibuka mshindi katika uchaguzi huu wa duru ya pili.