Umoja wa Ulaya na Canada zakubaliana kuhusu mkataba wa kibiashara, CETA
Nchi ya Ubelgiji hii leo imetangaza kufikiwa kwa makubaliano ambayo yatashuhudia yakifanikisha kutiwa saini kwa mkataba mkubwa wa kibiashara kati ya nchi za Ulaya na Canada, mkataba ambao awali ulikuwa kwenye hatihati.
Imechapishwa:
Makubaliano kuhusu mkataba huu yalikuwa ni muhimu kufikiwa, baada ya wananchi wa eneo la Wallonia nchini Ubelgiji kupiga kura ya hapana kuukataa mkataba kwa kile walichokuwa wakidai ni kupewa hakikisho kwanza la mustakabali wa viwanda vya eneo lao na wakulima wake.
Hata hivyo makubaliano haya yamefikiwa kwa kuchelewa kiasi ambacho kimewafanya viongozi wa umoja wa Ulaya na waziri mkuu wa Canada, Justin Trudeau kushindwa kuutia saini hivi leo kama ilivyokuwa imekubaliwa.
Waziri wa mambo ya nje wa Canada, Stephane Dion, amewapongeza wanasiasa nchini Ubelgiji kwa kufikia makubaliano, ambayo anasema sasa yatashuhudia yanazinufaisha pande hizo mbili kibiashara.
Mkataba huu utaliunganisha soko la umoja wa Ulaya lenye watu zaidi ya milioni 500 na kuwa soku kubwa zaidi duniani huku Canada ikiwa ni nchi ya 10 duniani yenye uchumi imara.
Waziri mkuu wa Ubelgiji Charles Michel ndiye aliyetangaza kufikiwa kwa makubaliano haya na viongozi wenzake wa mji wa Wallonia, ambao sasa wanaunga mkono mkataba huu unaofahamika kama CETA.
Mkataba huu sasa unasubiri kuungwa mkono na nchi zote 28 wanachama za umoja wa Ulaya kabla ya kutiwa saini katika tarehe ambayo itatangazwa baadae.