Mshambuliaji wa Munich ajiua baada ya kuua watu 9
Kijana mmoja raia wa Ujerumani mwenye asili ya Iran ambaye aliua watu tisa kwa kuwafyatulia risasi katika jumba moja la kibiashara mjini Munich,Ujerumani na kisha kujiua ameelezewa kutekeleza peke yake mauaji hayo kwa mujibu wa polisi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Polisi imeeleza hayo baada ya kuchunguza miongoni mwa waliofariki na kumbaini mtuhumiwa huyo aliyetajwa kuwa na umri wa miaka 18 ambapo imetoa ushauri kwa raia kutotoka nje.
Mauaji hayo yamesababisha Operesheni kubwa ya kiusalama kuanzishwa katika jumba la kibiashara la Olympia, ambalo linapatikana mtaa wa Moosach, kaskazini magharibi mwa Munich.
Awali Polisi ya Ujerumani, ambayo pia ilisema watu kadhaa wamejeruhiwa, inadhani kuwa washambuliaji watatu ndio wamehusika na shambulio hilo, na mpaka sasa haijulikani waliko.
Aidha "Mashahidi waliwaona watu watatu wenye bunduki, " polisi ya Munich imebaini kwenye Facebook. Wakazi wa mji wa Munich wametakiwa kusalia nyumbani. Eneo la kibiashara limezingirwa serikali imeendelea na zoezi la kuokoa watu waliokuwa ndani ya kituo hicho cha kibiashara.