Pata taarifa kuu
UBELGIJI-MASHAMBULIZI-UGAIDI

Ubelgiji: wahusika wa mashambulizi watambuliwa

Nchini Ubelgiji, Ofisi ya mashitaka imesema kuwa watuhumiwa wawili ambao ni ndugu wametambuliwa. Ndugu hao Khalid na Ibrahim El Bakraoui, walijilipua, mmoja katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Zaventem na mwengine katika kituo cha treni za mwendo wa kasi cha Maelbeek.

Picha kutoka kamera za ulizi za uwanja wa ndege wa Brussels-Zaventem ikionyesha watu watatu, wanaoshukiwa kuhusika katika mashambulizi ya Machi 22.
Picha kutoka kamera za ulizi za uwanja wa ndege wa Brussels-Zaventem ikionyesha watu watatu, wanaoshukiwa kuhusika katika mashambulizi ya Machi 22. AFP PHOTO / BELGIAN FEDERAL POLICE
Matangazo ya kibiashara

Mtuhumiwa wa tatu bado hajakamatwa na msako unaendelea katika eneo la Anderlecht. Idadi rasmi ya watu waliouawa katika mashambulizi hayo ni 31 na 270 wamejeruhiwa.

■ Ndugu wawili El Bakraoui

Mwendesha mashitaka Frédéric Van Leeuw amekua wazi Jumatano hii Machi 23: Ndugu wawili Ibrahim na Khalid El Bakraoui wametambuliwa kama washambuliaji wawili waliojitoa mhanga katika mashambulizi mawili yaliyotokea mjini Brussels Jumanne hii. "Magaidi wawili waliopoteza maisha walikua na rekodi ya uhalifu usiohusiana na ugaidi", Mwendesha mashitaka amesema.

Ibrahim El Bakraoui ametambuliwa kutokana na alama za vidole vyake kama mmoja wa wahusika wakuu wa mashambulizi katika uwanja wa ndege. Kwenye picha iliyopigwa na kamera za ulinzi (CCTV) za uwanja wa ndege wa Zaventem, Ibrahim El Bakraoui yupo katikati ya watu wawili. Picha hii imerushwa hewani kwenye vyombo vya habari.

Ndugu yake, Khalid El Bakraoui ametambuliwa, pia kutokana na alama za vidole vyake kama mhusika wa mashambulizi yaliotokea katika kituo cha treni cha Maelbeek katikati mwa mji mkuu wa Ulaya.

Wawili hawa pia ni ndugu wa karibu wa Salah Abdeslam, aliekamatwa Ijumaa, Machi 18. Utambulisho wao unathibitisha kwamba kuna uhusiano kati ya mashambulizi ya Paris na yale ya Brussels.

■ Kuwepo kwa washirika wengine?

Kuhusu picha iliyopigwa katika uwanja wa ndege wa Brussels: Mwanamume ambaye yupo upande wa kushoto hajatambuliwa. Mtu wa tatu ambaye amevaa kofia, upande wa kulia, yuko mafichoni, hajakamatwa, lakini operesheni ya kumsaka inaendelea. Aliacha mfuko kubwa uliojaa vilipuzi muhimu katika eneo la tukio, ambavyo vimeharibiwa na maafisa wa kutegua mabomu.

Wachunguzi pia wanatafuta kujua kama Najim Laachraoui, anaetuhumiwa kuhusika katika mashambulizi ya Paris na Saint-Denis, ni mmoja wa watu walioendesha mashambulizi katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Zaventem mjini Brussels. Chembe zake za damu zilipatikana kwenye kifaa cha kulipuka kiliotumiwa tarehe 13 Novemba mjini Paris.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.