Kamati ya umoja wa Mataifa yaamua kuwa Assange amewekwa kizuizini kinyume cha sheria
Serikali ya Uingereza inapinga uamuzi wa kamati maalumu ya umoja wa Mataifa iliyoamua kuwa mwanzilishi wa mtandao wa WikiLeaks, Julian Assange anazuiliwa kinyume cha sheria kwenye ubalozi wa Ecuador jijini London.
Imechapishwa:
Serikali ya Uingereza imesema kwenye taarifa yake kuwa, uamuzi wa kamati hiyo haubadili chochote, na kwamba inakataa kwa nguvu zote madai kuwa Julian Assange ni muhanga wa kushikiliwa kinyume cha sheria.
Taarifa ya Serikali imeongeza kuwa tayari wameweka wazi kwa kamati hiyo ya umoja wa Mataifa kuwa wanakataa ripoti mtazamo wao.
Tangazo hili la Serikali limekuja ikiwa ni muda mfupi tu umepita toka kamati ya umoja wa Mataifa iamue kuwa Julian Assange amekuwa akizuiliwa na maofisa wa Sweden na Uingereza kinyume cha sheria.
Uamuzi huu wa kamati ya umoja wa Mataifa umetoa matumaini mapya kwa Assange kuwa huenda akatoka nje ya ubalozi wa Ecuador akiwa huru baada ya kukaa hapo kwa karibu miaka minne.
Kamati hiyo kwenye uamuzi wake imeongeza kuwa, Assange anapaswa kufungua kesi ya madai dhidi ya Serikali ya Uingereza na Sweden toka muda alioomba hifadhi kwenye ubalozi wa Ecuador, ambako amekuwa hatoki nje, wala kukaa sehemu yenye mwanga.
Assange anatumaini kuwa uamuzi wa kamati hiyo licha ya kuwa sio lazima kwa Serikali ya Uingereza kuutekeleza, utaongeza shinikizo kwa Serikali ya Uingereza na Sweden kufuta mashtaka dhidi yake.
Kwenye taarifa yake aliyoitoa alhamisi ya wiki hii, Assange alisema kuwa baada ya uamuzi wa kamati hiyo, ataondoka kwenye ubalozi wa Ecuador na kwamba atakuwa tayari kukamatwa na maofisa wa Uingereza ikiwa kamati hiyo ingeamua kinyume na uamuzi wa hii leo.
Aliongeza kuwa uamuzi utakaoenda upande wake utamaanisha kuwa lazima aachiwe huru na vyombo vya usalama vya Uingereza pamoja na kurejeshewa pasi yake ya kusafiria.