Polisi Ufaransa waanza kuwabaini washambuliaji wakati huu taifa likiomboleza
Jeshi la polisi nchini Ufaransa limembaini mshambuliaji wa kwanza kati ya makundi matatu waliyojigawa washambuliaji hao katika kutekeleza mashambulizi mabaya zaidi kutokea nchini Ufaransa ambapo zaidi ya watu mia moja na ishirini wameuawa na mamia wengine kujeruhiwa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kundi la kijihadi la Islamic State limejigamba kutekeleza mashambulizi hayo katika mitaa kadhaa maarufu jiji Paris ikiwemo karibu na uwanja wa michezo wa taifa wa Stade de France ambako mechi ya kirafiki kati ya Ufaransa na Ujerumani ilikuwa ikiendelea.
Kati ya washambuliaji saba,sita walijilipua huku mmoja akizidiwa nguvu na polisi baada ya kumshambulia kwa risasi.Kundi hili lililojigawa katika makundi matatu na kutekeleza mashambulizi katika maeneo tofauti linakuwa kundi la kwanza kabisa kutekeleza mashambulizi ya kujitoa muhanga nchini Ufaransa.
Wanausalama kutoka Ufaransa Ubelgiji Ugiriki na Ujerumani tayari wameanza uchunguzi wa kuwabaini washambuliaji hao na jinsi gani walitekeleza mashambulizi ya kujitoa muhanga kwa ushirikiano na sababu za kufanya hivyo.
Hayo yanajiri wakati huu taifa hilo likiwa katika maombolezo ya siku tatu na hali ya hatari ikizingatiwa kama ilivyotangazwa na raisi Francois Hollande.